Simbu huyoo New York City Marathon

Muktasari:

  • Kocha wa mwanariadha huyo Francis John alisema tayari wamethibitisha mwaliko wake na mambo yote yanakwenda vyema huku taratibu nyingine za ruhusa zikiendelea kufanyiwa kazi kuona jinsi ya kufanya mazoezi.

ARUSHA. MKALI wa kufukuza upepo mwanariadha wa kimataifa kutoka Tanzania, Alphonce Simbu tayari ameanza kurejea katika mbio za ushindani baada ya kupata mwaliko wa kushiriki mbio za New York City Marathon zitakazofanyika Novemba 5.

Kocha wa mwanariadha huyo Francis John alisema tayari wamethibitisha mwaliko wake na mambo yote yanakwenda vyema huku taratibu nyingine za ruhusa zikiendelea kufanyiwa kazi kuona jinsi ya kufanya mazoezi.

“Kwa sasa yupo chini ya kocha Shabaan Hiki na tunaratajia kuanza programu yake kuelekea katika mbio hizo kwa maana muda uliobaki bado unatosha kutafuta pumzi na kasi,” alisema Francis.

Aliongeza kuwa katika akiwa anajiandaa na mbio hizo atahakikisha anashiriki mbio nyingi fupi za ndani ili kumrejeshea makali yake anapokutana na wanariadha chipukizi kutoka sehemu mbalimbali.

Bingwa wa mwaka jana katika mbio hizo alikuwa Geoffrey Kamworor aliyetumia muda wa saa 2:10:53 akifutwa na Mkenya mwenzake Lilisa Desisa aliyetumia saa 2:11:32 wakati Shalane Flanagan wa Marekani aliibuka kidedea kwa kinadada alikitumia saa 2:26:53 huku Mry Keitany wa Kenya ikimaliza wa pili akitumia saa 2:27:54.

Now York City Marathon iliyoanzishwa mwaka 1970 ni moja ya mbio kubwa Duniani ambayo rekodi ya muda hadi sasa inashikiliwa na wakenya Geoffrey Mutai aliyoiweka mwaka 2011 alipotumia saa 2:05:06 kumaliza mbio hizo, huku Magret Okayo akifanya hivyo kwa wanawake mwaka 2003 alipotumia saa 2:22:31.

Hata hivyo Mkongwe Juma Ikangaa naye anaingia kwenye rekodi ya kuwa na muda bora kwa Tanzania baada ya kufanya hivyo alipokuwa bingwa mwaka 1988 katika mbio hizo, lakini Samson Ramdhan nusura avunje rekodi hiyo mwaka 2003 katika michezo ya Jumuiya ya Madola alipotumia muda kama huo.