Simba yawatimua nyota 13, Okwi, Zana out

Muktasari:

Simba imesajili wachezaji 26 ambapo imebakiza nafasi moja ya kuongeza mchezaji kwa mujibu wa Magori ambayo itajazwa kabla dirisha la usajili alijafungwa.

Dar es Salaam. Simba imetangaza kuwaacha wachezaji wake 13, akiwemo mfungaji bora wa Uganda katika fainali za Afcon, Emmanuel Okwi.

Ofisa Mtendaji Mkuu wa Simba, Crescentius Magori alisema kati ya wachezaji hao, sita wametolewa kwa mkopo na saba wamemaliza mikataba.

"Waliomaliza mikataba klabu haikuhitaji kuendelea nao, isipokuwa Asante Kwasi ambaye mkataba wake unamalizika Novemba.

"Kwasi amepata timu na klabu tumeamua kuachana naye baada ya makubaliano ya pande zote mbili ili akaendelee na maisha mengine," alisema Magori.

Aliwataja wachezaji wengine walioachwa rasmi kuwa Haruna Niyonzima, Emmanuel Okwi, Nicholaus Gyan, Zana Coulibaly, Nicolaus Kotei na Salim Mbonde.

 

"Mbonde hatukutaka kumuacha, lakini mwalimu amependekeza kutokana na ushindani wa Simba ni bora aende kwenye timu nyingine ili akapate nafasi ya kucheza na kuendeleza kiwango chake," alisema Magori.

Wachezaji waliowatoa kwa mkopo ni Mohamed Ibrahim (Mo), Marcel Kaheza, Mohamed Rashid, Adam Salamba, Paul Bukaba na Abdul Athumani wa timu ya vijana ya U20.