Simba SC kung’oa mashine Mazembe

Muktasari:

Ourega aliwahi kuja hapa nchini mwezi Juni mwaka jana na alifanya majaribio ya wiki moja na Simba chini ya kocha Patrick Aussems ambaye alionyesha kutokuvutiwa na aina ya uchezaji wake ingawa pia ilidaiwa staa huyo alipigwa chini kutokana na kutoelewana kwa baadhi ya viongozi waliomleta na walioko kwenye uongozi.

TIMU pekee Tanzania iliyobeba vikombe vyote nchini msimu ulioisha, Simba inamnyemelea kiungo mkabaji wa TP Mazembe, Raia wa Ivory Coast, Jean Vital Ourega.

Ourega aliwahi kuja hapa nchini mwezi Juni mwaka jana na alifanya majaribio ya wiki moja na Simba chini ya kocha Patrick Aussems ambaye alionyesha kutokuvutiwa na aina ya uchezaji wake ingawa pia ilidaiwa staa huyo alipigwa chini kutokana na kutoelewana kwa baadhi ya viongozi wa-liomleta na walioko kwenye uongozi.

Wakati Ourega akiwa anafanya majaribio na Sim-ba, alikuwa tayari amepokea Dola 10,000 zaidi ya (Sh.20 milioni) kama advansi lakini baadaye ndiyo hivyo tena.Habari za uhakika zinasema kwamba wache-zaji wa Simba waliomuona kwenye majaribio ya mwaka jana walivutiwa naye na kushangazwa kwanini uongozi haukumsainisha.

Mazembe walimpa mkataba Ourega mwaka jana wakati Simba walipokuwa wakisuasua kumsainisha na sasa watalazimika kuingia gharama kumrejesha nchini kuongeza nguvu kwenye muziki wa Ligi ya Mabingwa Afrika.

Mwanaspoti inajua kwamba Simba wanapam-bana pia kumshusha straika, Mkongomani Chris Mugalu ambaye walikuwa wakimsaka tangu msimu uliopita ila walishindwa kumnasa kutokana na bajeti yake kuwa kubwa.

“Ourega amekubali kuja kucheza Simba msimu ujao lakini TP Mazembe wamesema hawatamuuza bali watamtoa kwa mkopo kwani mchezaji huyo bado ana mkataba na timu hiyo, kwa maana hiyo muda wowote kama mambo yatakwenda vizuri atawasili nchini,” alidokeza mmoja wa vigogo wa Simba.

Taarifa ambazo Mwa-naspoti inazo mpaka sasa Simba wamesajili wachezaji watatu, Charles Ilanfya kutokea KMC, David Kameta ‘Duchu’ kutoka Lipuli, Ibrahim Ame wa Coastal Union huku Bernard Morrison wa Yanga akiwa katika mvutano na waajiri wake Yanga kutokana na ishu ya kimkataba.

Kwa upande wa Ilanfya na Duchu walipozungumza na Mwanaspoti waliahidi kupambana na hawataridhika na mafanikio Simba.Nyota ambao wanaoachwa ni Rashid Juma ambaye bado ana mkataba na mabingwa hao ila anaweza kutolewa kwa mkopo na kuna baadhi ya timu kama Polisi Tanzania na nyinginezo zimeanza kuonyesha nia ya kutaka huduma yake.Wengine ni mabeki wa kati, Mbrazili Tairone Santos na Yusuph Mlipili wakati Haruna Shamte mwenye mkataba anaweza kuondoka jumla au kutolewa kwa mkopo Namungo.