Simba, Azam waanza tambo kiingilio buku tano tu

Muktasari:

Suala la vingilio itakua bei iliyozoeleka ambapo kila Tanzania ana uwezo wa kulipa ili kushuhudia mchezo huo

Dar es Salaam. Azam na Simba zimeanza kutambiana kuelekea katika mchezo wa Ngao ya Jamii utakaochezwa Jumamosi Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, huku kiingilio cha chini kikiwa ni shilingi elfu tano tu Sh5,000 tu.

Ofisa habari wa Azam, Jafari Maganga alisema kikosi chake kipo tayari kuikabili Simba licha ya kuwa watakosa huduma za wachezaji wap wawili, Mudathir Yahya na Aggrey Morris.

Maganga alisema anatambua kutakua na wingi wa mashabiki wa Simba katika mchezo huo hivyo haitakua sababu ya wao kupoteza mchezo huo kwa sababu wamejipanga vizuri.

“Tunawaheshimu Simba na tunaamini wanamashabiki wengi kutuzidi, lakini wachezaji wetu tumewajenga kucheza dhidi ya upinzani wenye mashabiki wengi hivyo hilo kwetu sio tatizo," alisema Maganga.

Naye Ofisa habari wa Simba, Haji Manara alisema timu ipo vizuri na inaendelea na mazoezi hivyo anawaomba mashabiki wa Simba kufika uwanjani na kuipa hamasa timu yao.

 “Wachezaji waliokuwa majeruhi wanaendelea vizuri huku Ibrahim Ajib na Aishi Manula wakiwa tayari wameanza mazoezi madogo madogo na ikimpendeza kocha atawatumia katika mechi dhidi ya Azam,” alisema Manala.

Afisa habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Clifford Ndimbo alizungumzia suala la vingilio kwa kusema kua itakua bei iliyozoeleka ambapo kila mtanzania ana uwezo wa kulipa.

“Kama ilivozoeleka kiingilio cha chini kitakua shilingi elfu tano ambapo ni fursa kwa watanzania wote kuweza kuingia na kutazama mchezo huo wa ngao ya jamii,” alisema Ndimbo