Phil Jones, Romero nje Man U UEFA

MANCHESTER, ENGLAND. WACHEZAJI watatu wa Manchester United wametemwa katika kikosi cha wachezaji 25 ambao watacheza michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya kwa msimu huu ikiwa pamoja na Sergio Romero Phil Jones na Marcos Rojo.

Licha ya wachezaji hao kuondolewa vyuma vyengine vipya vilivyosajiliwa katika dirisha lililopita ikiwa pamoja na Edinson Cavani, Facundo Pellistri na Alex Telles wamejumuishwa kikosini.

Romero, 33, alikuwa kwenye mpango wa kuondoka katika dirisha lililopita la usajili kujiunga na Everton, lakini mambo yalienda tofauti na kwa sasa anafikiria kutua moja ya timu za Ligi Kuu nchini Marekani.

Jones yeye ni miongoni mwa wachezaji ambao hawatakiwi na kocha Ole Gunnar Solskjaer na aliwekwa sokoni lakini hakuna timu iliyoonesha nia ya kutaka kumsaini.