Wakenya waweka rekodi mpya mbio za Valencia

Muktasari:

Kipruto alishinda mbio za kilomita 10 za Valencia Ibercaja akitumia muda wa dakika 26:23, huku Chepkirui akishindakwa wanawake akitumia muda wa dakika 29:42.

Nairobi. Mkenya Rhonex Kipruto mshindi wa medali ya shaba katika mbio za Dunia katika mita 10,000 pamoja na Bingwa wa Afrika wa mbio za mita 5000 (2016), Sheila Chepkirui wamevunja rekodi ya Dunia ya mbio za barabarani za kilomita 10, kwa wanaume na wanawake zilizofanyika jijini Valencia nchini Hispania.

Kipruto, mwenye umri wa miaka 20, alishinda mbio za kilomita 10 za Valencia Ibercaja, akiweka rekodi mpya ya Dunia, alipotumia muda wa dakika 26:23, kuvuka utepe, huku Chepkirui, ambaye ni mshindi wa fedha wa Afrika wa mwaka 2016, katika mashindano za mbio za nyika, akitumia muda wa dakika 29:42, kuweka rekodi mpya ya Dunia, kwa upande wa wanawake.

Kipruto ni bingwa wa U20 wa Dunia, mbio za mita 10,000, aliweka rekodi hiyo mpya, akivunja rekodi ya bingwa wa Dunia, iliyokuwa ikishikiliwa na Mganda Joshua Cheptegei aliposhinda mbio za Half Marathon, mjini Valencia, wiki sita zilizopita (Desemba mosi).

Chepkirui yeye alivunja rekodi ya Mkenya mwenzake, Joyciline Jepkosgei, ambaye ni bingwa wa Marathon wa New York wa mwaka 2019.

Jepkosgei aliweka rekodi ya dakika 29:43, aliposhinda mbio Birell Prague Grand Prix, zilizofanyika Septemba 2017, nchini Czech, kabla ya Chepkirui kutumia sekunde moja kuivunja.

Matokeo ya Wanaume:

1. Rhonex Kipruto (Kenya) 26:24 (WR)

2. Bernard Kimeli (Kenya) 27:12

3. Julián Wanders 27:13 (AR-Europa)

 

Matokeo ya Wanawake:

1. Sheila Chepkirui (Kenya) 29:42

2. Rosemary Wanjiru (Kenya) 29:46

3. Norah Jeruto (Kenya) 29:46