Manchester United yafungua mlango kwa Pogba kuondoka

Muktasari:

Pogba amekuwa nje ya uwanja kwa muda mrefu akiunguza majeraha ya kifundo cha mguu

London, England.Manchester United imefungua milango kwa kiungo Paul Pogba kuondoka baada ya kuweka wazi mpango wa kuwasajili viungo wawili msimu ujao Saul Niguez na Donny van de Beek.

Kiungo Pogba bado anaonyesha anataka kuondoka akilazimisha uhamisho wa kwenda Barcelona na Real Madrid klabu zinazoonyesha nia ya kumtaka kwa zaidi ya miaka miwili sasa.

Mfaransa huyo amebakiza miezi 18, katika mkataba wake wa sasa unampa mshahara wa pauni 290,000 kwa wiki, japokuwa Man United wanayonafasi ya kuongeza mwaka moja zaidi hadi Juni 2022.

Klabu hiyo mwanzoni mwa msimu huu ilifanya juhudi kubwa kuzungumza na Pogba kuhusu kuongeza mkataba, lakini wakala wake hakuwa tayari kujadili suala hilo hadi sasa.

Hata hivyo kocha wa Manchester United, Ole Gunnar Solskjaer amekuwa akisisitiza kuwa kiungo huyo mwenye miaka 26, hauzwi. Lakini mpango wake wa kutaka kusajili viungo wawili wa kati na mshambuliaji katika usajili ujao inatoa ishara kwamba wanajianda kuacha na Mfaransa huyo.

Wachezaji wanaotaka kuwasajili ni pamoja na kiungo wa Ajax, Donny van de Beek na nyota wa Atletico Madrid, Saul Niguez, pamoja na mshambuliaji wa Red Bull Salzburg, Erling Braut Haaland ambaye wanafanya kazi chini ya wakala Mino Raiola pamoja na Pogba.