Manchester City, Arsenal, Aston Villa ya Samatta zapata sare

Muktasari:

Sare hiyo inaifanya Manchester City kuwa nyuma kwa pointi 13, nyuma ya vinara wa ligi hiyo Liverpool ambao kesho watacheza dhidi ya Manchester United.

London, England. Mabingwa watetezi Manchester City na Arsenal zimelazimishwa sare nyumbani na Crystal Palace na Sheffield United katika michezo ya Ligi Kuu England iliyofanyika leo.

Manchester City imeweka rehani ubingwa wake baada ya kiungo wake Fernandinho kujifunga katika dakika 90 na kuipa pointi moja Crystal Palace sare 2-2 kwenye Uwanja wa Etihad.

Mshambuliaji Sergio Aguero alifunga mabao mawili katika dakika 10 za mwisho baada ya Palace kupata bao la mapema katika kipindi cha kwanza lililofungwa na Cenk Tosun.

Wageni Palace walisawazisha baada ya Wilfried Zaha kupiga krosi iliyomgonga Fernandinho na mpira kuingia wavuni.

Sare hiyo inaifanya Manchester City kuwa nyuma kwa pointi 13, nyuma ya vinara wa ligi hiyo Liverpool ambao kesho watacheza dhidi ya Manchester United.

Arsenal ikiwa nyumbani imepoteza pointi baada ya kulazimishwa sare 1-1 na Sheffield United kwenye Uwanja wa Emirates.

Wenyeji Arsenal ilipata bao kuongoza dakika 45 kupitia Gabriel Martinelli, lakini Sheffield ilisawazisha dakika 83, kupitia kwa John Fleck.

Katika michezo mingine Aston Villa inayosaka saini ya Mtanzania Mbwana Samatta imelazimisha sare 1-1 na Brighton ugenini.

Jahazi la Jose Mourihno bado linaendelea kuyumba baada ya Spurs kulazimishwa suluhu na Watford.

Norwich imepata ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Bournemouth wakati Southampton wakiwa nyumbani walikubali kipigo cha mabao 3-2 kutoka kwa Wolves, huku West Ham ikilazimishwa sare 1-1 na Everton.