Kisa Vyombo: King Dodoo awashukia wanaomponda Christian Bella

Muktasari:

Christian Bella ni mwanamuziki, yupo chini ya kampuni inaitwa Kwete King Dom inayosimamia masuala yote ya muziki wa mwanamuziki huyo.

Dar es Salaam.Meneja wa mwanamuziki Christian Bella, King Dodoo ameshangazwa na watu kumbeza Bella kwa kushindwa kumiliki vyombo vyake vya muziki wa dansi.

Kauli hiyo ya Dodoo imekuwa baada ya mwanamuziki wake Bella kushindwa kufanya shoo katika mkesha wa mwaka mpya kwenye ukumbi wa PK Kimara Korogwe hadi mmiliki wa ukumbi huo kufungia vyombo vya muziki ambavyo ni mali ya mwanamuziki Mafumu Bilali.

Akizungumzia sakata hilo Dodoo alisema kutokuwa na vyombo vya muziki ni uamuzi wa mtu, sisi bado hatuitaji vyombo maana hatutaki 'stress', ukitulipa show tukitoa fedha ya vyombo hatupati 'stress' sasa tukiwa na vyombo nilazima uhakikishe unakata hela ya matunzo ya vyombo.

"Kwanza naomba niulizie watu wanaojua muziki duniani hivi mwanamuziki gani mkubwa wameona ana vyombo vya muziki? hivi unaweza kujua R kelly ana vyombo? Michael Jackson ana vyombo? Jay Z ana vyombo? halafu niulizie hapa Tanzania wanitajie mastaa gani wa muziki wana vyombo vya kwake? basi wajue huko ndio kwenye Dunia" alisema King Dodoo

Aidha king Dodoo aliongeza kwa kusema watu wanatakiwa watambue kitu kimoja kuwa Christian Bella ni mwanamuziki, lakini yupo chini ya kampuni ambayo kampuni hiyo inaitwa Kwete King Dom, ni kampuni ambayo imesajiliwa kihalali na inalipa kodi.

Alisema hiyo kampuni ina wakurugenzi wake na ndio inapanga mambo yote na inatakiwa kujua kila anachofanya Bella kinalipa kiasi gani, hivyo wao wanaenda kimahesabu na wanajua wanachokifanya.