JKT Tanzania yaichapa Alliance ndani Nyamagana

Muktasari:

Huo ni mchezo wa tatu kwa Alliance kupoteza kwenye uwanja wa Nyamagana baada ya Kagera Sugar iliyoshinda 2-1, Azam 5-0 na leo kulala 1-0

Mwanza. Bao la Edson Katanga katika dakika ya 16, limetosha kuipa JKT Tanzania pointi tatu muhimu kwa kuichapa Alliance 1-0 katika mchezo wa Ligi Kuu Bara uliopigwa leo Jumatano kwenye Uwanja wa Nyamagana, Mwanza.

Ushindi huo umeifanya JKT Tanzania kufikisha pointi 26 huku Alliance ikibaki nafasi ya 15 na pointi zake 20.

JKT Tanzania ilitawala mchezo huo yangu mwanzo kwa kufanya mashambulizi mengi langoni mwa Alliance walionekana wakicheza kwa kujilinda zaidi.

Katika mchezo huo Alliance iliwakosa nyota wake mkongwe, Jerryson Tegete na Chinedu Michael na kuliacha jahazi chini ya Ally Lucha aliyekuwa akicheza kwa mara ya kwanza.

Katika kipindi cha pili, Alliance walibadili mbinu na kufanya mashambulizi ya kushtukiza, lakini ngome ya JKT Tanzania ilikuwa makini kuokoa hatari hizo.