Dude: Wanaume wasiwe kichwa cha familia

Muktasari:

Mfumo dume ndio chanzo cha akina baba wengi kupoteza maisha haraka kutokana na mlindikano wa majukumu na msongo wa mawazo

Dar es Salaam. Mwingizaji wa Bongo Movie Tanzania, Dude amesema mfumo wa sasa wa mwanaume kuonekana kichwa cha familia ni mbaya na hautakiwi kuendelezwa kwani unafanya mwanaume kuchoka haraka.

Dude jina lake halisi ni Kulwa Kikumba amedai katika familia lazima kuwe na usawa wa kijinsia ili wanawake na wanaume wote wawe na haki sawa ya kuijenga familia.

Akitolea mfano wa familia yao, Dude ambaye kipindi chake cha maigizo kinachoitwa 'Bongo Dar es Salaam chenye maudhui ya utapeli' kwa sasa kinarushwa Wasafi Tv amesema baba yake mzazi alikuwa ndio kichwa cha familia jambo ambalo lilifanya yeye kuwa mtu wa mwisho kutoa uamuzi.

“Baba yangu alikua kichwa cha familia mwamuzi wa mwisho, mimi nataka kua baba wa familia ambayo wazazi wote wawili ndio vichwa vya familia na wanaamua kwa kukubaliana, Mzee wangu ni picha halisi ya mfumo dume mimi nataka kua picha halisi ya usawa wa jinsia.”  amesema Dude

Aidha Dude amesema kuwa mfumo dume ndio chanzo cha akina baba wengi kupoteza maisha haraka kutokana na mlindikano wa majukumu na msongo wa mawazo, jambo linalopelekea kuongezeka kwa wajane.