Azam yamnasa kiungo wa Platinums ya Zimbabwe

Muktasari:

Never anaweza kucheza nafasi ya namba sita, nane na saba, hadi anaondoka Platnum amefanikiwa kuifungia mabao manne kwenye Ligi ya mabingwa Afrika ambayo iliingia hatua ya makundi ya michuano hiyo mwaka huu

Dar es Salaam. Uongozi wa klabu ya Azam Fc umekamilisha usajili wa kiungo wa kimataifa wa Zimbabwe, Never Tigere kwa mkataba wa mwaka mmoja akitokea klabu ya Fc Platinums.

Kiungo huyo alisaini rasmi mkataba jana usiku (Jumatatu) baada ya kutua tu akitokea nchini Zimbabwe na moja kwa moja alipelekwa katika ofisi za Mzizima na kukutana na Mtendaji mkuu Abdulkarim Amin ‘Popat’ na kumaliza dili hilo.

Never anaweza kucheza nafasi ya namba sita, nane na saba, hadi anaondoka Platnum amefanikiwa kuifungia mabao manne kwenye Ligi ya mabingwa Afrika ambayo iliingia hatua ya makundi ya michuano hiyo mwaka huu.

Katika eneo la kiungo ukabaji Azam, Never atakutana na changamoto ya namba kutoka kwa Mudathir Yahya na Frank Domayo wanaocheza nafasi hiyo.

Huu ni usajili wa pili kwa Azam Fc katika dirisha dogo la usajili baada ya mwanzo kumsajili Khleffin Hamdoun kutoka Mlandege, Zanzibar.