Manchester United yaichapa Watford yapaa England

Muktasari:

Kwa matokeo hayo Manchester United sasa wamefufua matumaini ya kushiriki michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya msimu ujao.

MANCHESTER, ENGLAND. MANCHESTER United imepanga kutoka nafasi ya saba hadi ya tano katika msimamo wa Ligi Kuu England baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Watford katika mchezo mkali uliopigwa katika Uwanja wa Old Trafford.

Katika mchezo huo mabao ya Manchester United yaliwekwa kimiani na Bruno Fernandes, Anthony Martial na Meson Greenwood, huku timu hiyo ikionyesha kiwango cha juu dhidi ya Watford ambao wako kwenye hatari ya kushuka daraja.

Alikuwa Fernandes ambaye aliipatia Manchester United bao la kwanza kwa njia ya penalti katika dakika ya 42 ya mchezo huo, penalti ambayo iliyotakana kipa wa Watford, Ben Foster kumfanyia madhambi kiungo huyo katika eneo la hatari.

Bao la pili la Manchester United liliwekwa kimiani na Martial kwa juhudi binafsi katika dakika ya 58 ya mchezo huo, huku kinda Greenwood akifunga bao la tatu katika dakika ya 75 akimalizia pasi safi ya Fernandes.

Kwa matokeo hayo Manchester United sasa wamefufua matumaini ya kushiriki michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya msimu ujao.