Azam FC yaifuata Ihefu kutetea ubingwa wake wa Kombe la FA

Muktasari:

Ihefu itacheza mchezo wa Kombe la Fa na Azam Fc Jumatano kwenye Uwanja wa Sokoine, Mbeya.

Dar es Salaam. Klabu ya Azam FC imeondoka leo Jumatatu kwenda mkoani Mbeya tayari kwa mchezo wake wa hatua ya 16 bora ya Kombe la Shirikisho ASFC dhidi ya Ihefu.

Azam mabingwa watetezi wa kombe hilo, wameondoka leo Jumatatu kwa usafiri wa gari kwenda mkoani Mbeya kuwakabili Ihefu.

Kupitia kwa Afisa Habari wa klabu hiyo, Jaffer Idd alisema kikosi hiko kinakwenda katika mchezo huo wakiwa wanahitaji kuendelea kutetea ubingwa wao.

"Mwalimu tayari ameshachagua wachezaji ambao wanaenda katika mchezo huu kwaajili ya kwenda kupambana kuhakikisha wanatetea taji," alisema.

Aliongeza kwa kusema anatambua ugumu wa mechi hiyo kwani Ihefu wanaongoza Kundi A katika Ligi Daraja la Kwanza wakiwa na pointi 30 sawa na Dodoma Fc.

"Ihefu ni timu nzuri na wanaongoza katika kituo chao huko, mchezo utakuwa mzuri lakini tunajua umakini unaowekwa na wachezaji wetu," alisema.

Ihefu itacheza mchezo wa Kombe la Fa na Azam Fc Jumatano kwenye Uwanja wa Sokoine, Mbeya.