Mwakinyo apigia hesabu ubingwa wa dunia

Muktasari:

Mwakinyo hivi sasa ni bingwa wa Universal Boxing Organization (UBO) International alioshinda mwaka 2018 kwa kumchapa Joseph Sinkala

Dar es Salaam. Bondia Hassan Mwakinyo ameanza kupiga hesabu ya kuwania mkanda wa ubingwa wa dunia 2020.

Mwakinyo ambaye hivi karibuni alimchapa Arnel Tinampay kwa pointi za majaji 2-1 jijini Dar es Salaam amesema malengo yake sasa ni kuwania ubingwa wa dunia.

"Mpango uliokuwepo ni kwamba mshindi kati yangu na Tinampay ataandaliwa pambano la ubingwa, hivyo harakati hizo ndizo zimeanza sasa," alisema bondia huyo.

Alisema hivi sasa yuko kwenye mapumziko mafupi baada ya pambano na Tinampay na hivi karibuni ataanza mazoezi kujiandaa na pambano hilo.

"Nitajipanga ili kufanya vizuri zaidi kwenye pambano hilo, najua mashabiki wangu walitarajia nimchape Tinampay kwa KO (knock out), lakini ikawa ndivyo sivyo.

"Mpinzani wangu alikuwa bondia mgumu, japo nilishinda lakini kwa tabu, hivyo sitopenda ijirudie nitakapokuwa nikicheza pambano la ubingwa.