Mwakinyo ajipange kulinda hadhi na heshima

Muktasari:

Kwa wanaokumbuka miaka hiyo ngumi zilikuwa zikijaza mashabiki ukumbini na kuwa na amsha amsha kama pambano ya soka, mchezo unaoatajwa kuwa na mashabiki wengi na kufuatiliwa kwa karibuni nchini.

MASHABIKI na wapenzi wa mchezo wa ngumi hususani zile za kulipwa, wanahesabu saa tu kabla ya kushuhudia pambano la kimataifa la raundi 10 la uzani wa Super Welter.

Bondia Mtanzania, Hassan Mwakinyo atapanda ulingoni kesho Ijumaa dhidi ya Arnel Tinampay kutoka Ufilipino katika pambano lisilio la ubingwa lakini mwenye kuonyesha heshima na hadhi kwa mabondia wote wawili. Mwakinyo anayeshika nafasi ya kwanza Afrika kwa uzani huo na wa 19 duniani akiwa pia ndiye kinara kwa hapa nchini kwa sasa yupo daraja la nyota nne na akishinda ataingia katika nyota tano, ilihali Mfilipino anayeongoza nchini kwao anataka kupanda kutoka nyota mbili alizonazo sasa. Leo Alhamisi mabondi hao na wale watakaowasindikiza watapima uzito kabla ya mapambano yao ya kesho jkwenye Uwanja wa Uhuru, jijini Dar es Salaam huku mashabiki wakijadili pambano hilo, baadhi wakiamini Mwakinyo ataendeleza rekodi za kuibabe na wengine wakidhani atapigwa.

Kifupi ni kwamba hamasa ya kuelekea pambano hilo imekuwa kubwa na kuonyesha namna gani mchezo wa ngumi ulivyo na mashabiki, isipokuwa kuna mambo yanakosewa katika kuuweka kwenye kiwango cha juu kama ilivyokuwa miaka ya 1990-2000.

Kwa wanaokumbuka miaka hiyo ngumi zilikuwa zikijaza mashabiki ukumbini na kuwa na amsha amsha kama pambano ya soka, mchezo unaoatajwa kuwa na mashabiki wengi na kufuatiliwa kwa karibuni nchini.

Enzi hizo mapromota na waandaaji wenye majina kama DJB ya kina Dioniz na Jamal Malinzi, Don King na wengine walifanya ngumi kuwa na mvuto na hata mabondia waliokuwa wakipigana walikuwa wakivutia mashabiki kama ilivyokuja kuwa kwa kina Francis Cheka, Karama Nyilawila, Thomas Mashali na wengine wa kiama ya karibuni.

Mwakinyo kama ilivyo kwa Dulla Mbabe, Mfaume Mfaume na Ibrahim Class wameanza kurejesha ile ladha na kilichobaki ni kwa mapromota na waandaaji kukazia hapo kwa kuleta mapambano yenye msisimko kama hilo la Mwakinyo na Tinampay.

Hata hivyo, tunaamini hii ni changamoto kwa Mwakinyo kuhakikisha anapata matokeo mazuri dhidi ya mpinzani wake, ili kuzidi kuwavuta hata wale wasiopenda ngumu kuanza kuzifuatilia. Matokeo mazuri yatazidi kuliweka jina lake kwenye matawi ya juu, lakini pia kuvutia hata makampuni na taasisi nyingine kujimwaga kudhamini mapambano ya ngumi na kurejesha ile hadhi iliyokuwa nayo miaka ya nyuma kabla ya kufifia na kuibuka upya hivi karibuni.

Kufanya vibaya kwa mabondia wa Tanzania mbele ya wageni ni mja ya sababu zinazochangia kufanya ngumi zodorore, ndio maana tunamkumbusha Mwakinyio pambano lake la kesho kama alivyolipa kauli mbinu yake ya ‘do or die’, ni lazima afanye kweli.

Licha ya tambo zake kwamba amejiandaa kumpiga Tinampay mapema, lakini ngumi sio rahisi kihivyo na kwa kurejea rekodi za mabondia kutoka Ufilipino zinaweza kumpa wakati mgumu kama hatajipanga vizuri. Tunamtakia kila la heri Mwakinyo kwenye pambano hilo kwa kumsisitiza ajue Watanzania wapo nyuma yake, huivyo asipande ulingoni akimdharau mpinzani wake ili asipate aibu, lakini pia atambue ushindi wa kesho ni heshima kwake na Tanzania kwa ujumla.