Mtibwa yampa Katwila maumivu

Dar es Salaam. Vichapo katika mechi tatu mfululizo vinamuumiza kichwa kocha wa Mtibwa Sugar, Zubery Katwila, ambaye amepanga kutafuta sababu ya hilo.

Katwila alisema jana kuwa kabla ya mechi wamekuwa na mipango mizuri ya ushindi, lakini wakiingia uwanjani mambo yanakuwa tofauti, hivyo anatakiwa kulifanyia kazi jambo hilo haraka.

Mtibwa Sugar katika mechi sita ilizocheza hadi sasa imeambulia pointi tano, huku ikichapwa mechi tatu mfululizo dhidi ya Yanga (1-0), Biashara (1-0) na juzi ikifungwa mabao 2-0 dhidi ya Gwambina.

“Pointi tano mechi sita si mwenendo mzuri kwetu kwenye ligi, tunatakiwa kubadilika.

“Tutajitahidi kuangalia nini tatizo ambalo linasababisha tunapoteza michezo yetu mfululizo ili kuhakikisha tunalitatau mapema tunafanya vizuri mechi zijazo.

“Tunaingia katika mechi tukiwa na mipango mizuri ya mchezo, lakini mwisho tunajikuta tunapoteza, hivyo kuna kitu hakiko sawa inabidi tukifanyie kazi haraka ili mambo yasiwe mabaya,” alisema Katwila.

Mtibwa Sugar imeanza ligi msimu huu kama ilivyoanza msimu uliopita kwani hata msimu uliopita ilikusanya pointi tano katika mechi sita za awali ikishinda moja, sare mbili na kupoteza michezo mitatu.

Msimu uliopita ilinusurika kushuka daraja kutokana na mwenendo mbovu