Mnamibia wa Yanga aitaja Simba tukutane uwanjani

Muktasari:

Mshambuliaji mpya wa Yanga, Sydney ametua jijini leo Jumanne tayari kuifanyia kazi klabu hiyo.

Dar es Salaam. Mshambuliaji wa Yanga, Sydney Urkhob ameitaja Simba na kusema anawaheshimu ila mambo yake watayaona uwanjani.

Sydney ametua Dar es Salaam leo Jumanne akitokea kwao Namibia alipokelewa na Ofisa Habari Msaidizi wa Yanga, Godlisten Chicharito na kuondoka naye kwenda Morogoro, kambini.

Akizungumza kushindwa kwake kupata nafasi katika kikosi cha Simba msimu uliopita Urkhob alisema mpambanaji hawezi kukaa na kulia akiitaja Simba, lakini atahakikisha anafanya kazi nzuri kwa ajili ya Yanga.

"Simba timu kubwa siwezi kuzungumza kibaya kwao, lakini watu watambue nimekuja Yanga kwa ajili ya kufanya kazi na ndio majukumu yangu kuhakikisha inafikia malengo tuliyokusudia na timu yangu," alisema Sydney.

Mshambuliaji huyo amekwenda Morogoro kuungana na kikosi cha Yanga ambacho kinafanya maandalizi yao huko kwa ajili ya msimu wa Ligi Kuu Bara na mashindano mengine.