Minziro aitabiria makubwa Singida United

Kocha wa Singida United, Fred Felix Minziro

Dar es Salaam. Kocha wa Singida United, Fred Felix Minziro amesema ana matumaini makubwa ya kikosi chake kufanya vizuri msimu ujao wa Ligi.
Singida United ambayo msimu uliopita ilimaliza Ligi ikiwa nafasi ya 13 imepiga kambi jijini Mwanza kwa ajili ya maandalizi ya msimu mpya wa Ligi.
Akizungumzia maandalizi yao, kocha Minziro alisema amewapima vijana wake katika mechi kadhaa za kirafiki ambapo wameonyesha matumaini ya kufanya vizuri msimu ujao.
"Bado nahitaji kucheza mechi nyingine tatu zaidi za kirafiki ili kuwajenga vijana wangu kabla ya msimu kuanza, naamini kwa maandalizi tunayoyafanya sina shaka kwamba tuaanza msimu vizuri na hata kumaliza Ligi katika nafasi nzuri zaidi," alisema.
Msimu uliopita, Singida United ilishinda mechi 11 ambazo tisa ilishinda nyumbani kwenye uwanja wa Namfua na kutoka sare mechi 13, sita zikiwa za nyumbani na kufungwa michezo 14, 10 ikiwa ugenini ambapo ilimaliza Ligi ikiwa na pointi 46,  33 ikivuna nyumbani na 13 ugenini.