McTominay, Maguire wanapiga mzigo kinoma

Muktasari:

Hata hivyo, kiungo huyo wa kati wa Scotland hatakuwamo uwanjani kesho Jumapili wakati timu yake itakapoikabili Sheffield United kutokana na kuwa majeruhi, lakini ukweli ndiye mchezaji aliyekimbia umbali mrefu zaidi, akipiga kilomita 130.9.

MANCHESTER, ENGLAND . SCOTT McTominay na Harry Maguire ndio wachezaji wanaopiga mzigo mkubwa zaidi kwenye kikosi cha Manchester United kwa msimu huu, kwa mujibu wa takwimu zao.

Unaambiwa hivi kwenye kikosi hicho cha wababe wa Old Trafford ni wachezaji watano tu waliokimbia kuvuka kilomita 100 ndani ya uwanjani kwenye mikikimikiki ya Ligi Kuu England msimu huu.

Zikiwa zimechezwa mechi 12 tu, kiungo McTominay ndiye mchezaji aliyekimbia eneo kubwa zaidi ndani ya uwanja, huku beki wa kati Maguire akishika namba mbili kwa mastaa wa Man United waliokimbia umbali mrefu ndani ya uwanja kwenye ligi hiyo.

Hata hivyo, kiungo huyo wa kati wa Scotland hatakuwamo uwanjani kesho Jumapili wakati timu yake itakapoikabili Sheffield United kutokana na kuwa majeruhi, lakini ukweli ndiye mchezaji aliyekimbia umbali mrefu zaidi, akipiga kilomita 130.9.

Beki, Maguire, aliyenaswa kwa Pauni 85 milioni akitokea Leicester City katika dirisha la uhamisho lililopita, amekimbia jumla ya kilomita 112.2 uwanjani huku pia akiwa ndiye nguzo kuu ya safu ya ulinzi kwenye kikosi hiki, huku Daniel James, akiwa amekimbia kilomita 107.8, Marcus Rashford kilomita 105.2 na anayekamilisha tano bora ni Andreas Pereira, aliyekimbia kwa kilomita 101.6.

Kwa wachezaji wenye kasi, straika Rashford ndiye aliyewazidi wenzake, akikimbia spidi ya mita 22.6 kwa saa na kumpiku James, ambaye mkongwe Ryan Giggs, alidai ana kasi kuliko mchezaji yeyote aliyepata kumwona, amekimbia kwa spidi ya mita 21.8 kwa saa.