Mawenzi Market, Sahare All Stars, Green Warriors zampa hofu kocha Stand United

Muktasari:

Stand United ipo nafasi ya 10 na pointi 20 huku Mawenzi Market (21), Sahare All Stars (19), Green Warriors wakiburuza mkia katika Kundi B na pointi 18.

Mwanza. Wakati Ligi Daraja la kwanza ikiwa imebakisha mechi nne kumalizika Kocha wa Stand United, Aguto Manyundo amesema ana kazi nzito ya kupambana na timu tatu ili kukwepa janga la kushuka msimu huu.

Stand United ipo nafasi ya 10 na pointi 20 huku Mawenzi Market (21), Sahare All Stars (19), Green Warriors wakiburuza mkia katika Kundi B na pointi 18.

Manyundo alisema ana kazi nzito ya kupambana na timu hizo tatu zizonataka kujinasua wasishuka daraja hivyo anatakiwa kukomaa ipasavyo kuhakikisha wanabaki.

Alisema wamebakiza mechi nne moja wanacheza nyumbani na tatu zote watazicheza ugenini kitu ambacho wanatakiwa kupambana vilivyo kupata ushindi kwenye mechi hizo.

Kocha huyo alisema kwake hajawahi kuishusha timu daraja hivyo atakomaa ili Stand United ibaki msimu ujao kwani hataki kuona rekodi zake zinachafuka.