Mastaa anaowaiga Pogba kama wote

Muktasari:

  • Wakati sasa akionekana kufurahia soka lake huko kwenye kikosi cha Man United tangu kocha Jose Mourinho alipofutwa kazi na mikoba kuchukua Ole Gunnar Solskjaer, Pogba alisema wakati anakua alikuwa akijifunza kwa kuwatazama Zinedine Zidane na Cristiano Ronaldo, kabla ya kuwafuatilia wachezaji wengine ambao, pia amekuwa akijitahidi kuiga mambo yao uwanjani.

MANCHESTER, ENGLAND.SUPASTAA wa Manchester United, Paul Pogba amesema kuna mastaa sita ambao siku zote amekuwa akiwatazama hao na kutaka kucheza soka lake kwa kufuata nyayo zao.

Sambamba na hilo, Pogba amesema pia kuna washambuliaji wengine watatu ambao, amekuwa akijifunza kupitia wao ili kuwa bora zaidi.

Wakati sasa akionekana kufurahia soka lake huko kwenye kikosi cha Man United tangu kocha Jose Mourinho alipofutwa kazi na mikoba kuchukua Ole Gunnar Solskjaer, Pogba alisema wakati anakua alikuwa akijifunza kwa kuwatazama Zinedine Zidane na Cristiano Ronaldo, kabla ya kuwafuatilia wachezaji wengine ambao, pia amekuwa akijitahidi kuiga mambo yao uwanjani.

“Nilipokuwa mdogo, nilikuwa nashambulia sana hivyo nilikuwa nikiwatazama Ronaldinho, (Zinedine) Zidane na (Cristiano) Ronaldo, hao wote ni wachezaji wa kushambulia,” alisema Pogba.

“Kwa sasa nawatazama Kevin De Bruyne, (Luka) Modric na Toni Kroos. Baada ya hapo, ninachojaribu ni kuwa mimi, najaribu kuwa tofauti nikifanya mambo yangu uwanjani kimchanganyiko kwa kutazama vitu vya Steven Gerrard, (Mesut) Ozil, Frank Lampard.”

Pogba amefikisha mabao 11 kwenye Ligi Kuu England msimu huu, lakini amekuwa moto zaidi wa kuotea mbali tangu kikosi hicho cha Old Trafford kilipoanza kuwa chini ya Solskjaer.