Manchester United, Ousmane Dembele ni suala la muda tu

MANCHESTER United imefikia hatua nzuri kukamilisha mchakato wa kuinasa saini ya kiungo wa Barcelona na timu ya taifa ya Ufaransa, Ousmane Dembele, 23, katika dirisha hili la usajili wa majira ya wachezaji.

Barcelona inataka kumuuza mchezaji huyo ili kupata fedha za kumsainisha winga wa Olympique Lyon, Memphis Depay ambaye ni chaguo la kocha Ronald Koeman.

Dili hilo huenda likakamilika kabla ya wiki hii kwisha na Man United itatakiwa kutoa kiasi kisichopungua Euro 60 milioni. Mkataba wa Dembele unatarajiwa kumalizika 2023 huku thamani yake katika soko la usajili ikiwa Euro 56 milioni.

Mchezaji huyo hajaonyesha kiwango kilichotarajiwa tangu asajiliwe 2017 kwa ada ya Euro 133 milioni akitokea Borussia Dortmund na shida kubwa ni majeraha ya mara kwa mara anayokumbana nayo uwanjani.