Manara awaonya wanaotaka kuuza jezi feki za Simba

Muktasari:

Simba ni miongoni mwa klabu zinazonufaika na mauzo ya jezi inadaiwa kuingiza zaidi ya Sh200milioni kwa mwaka ikiwemo na mauzo ya mabegi.

Dar es Salaam. Uongozi wa Simba umewaonya walanguzi wa jezi kufuatia kuingizwa nchini kwa mzigo jezi unadaiwa kutoka Asia bila ya kutambuliwa na klabu hiyo.

Akizungumza leo ofisa habari wa Simba, Haji Manara alisema wameandika barua kwa mamlaka kusika ili kuwadhibiti walanguzi hao.

Manara aliyasema hayo kwenye mkutano na waandishi wa habari alipokuwa akizungumzia maandalizi ya mechi ya Ngao ya Jamii kati ya Simba dhidi yaa Azam utakaochezwa Jumamosi kwenye Uwanja wa Taifa.

"Kama kuna watu wanataka kuuza jezi zetu wafuate taratibu na sio kuamua kutengeneza jezi feki, nilipokuwa nikija hapa niliambiwa nilisisitize hilo.

"Namna nzuri ya kuwadhibiti walanguzi nadhani ni kuzuia mizigo yao hadi pale ambapo yanafanyika mawasiliano na klabu ili kutambua kama kuna mahusiano yoyote.

Manara aliongeza,"tusije kupeana lawama Jumamosi kwa yeyote atakayekutwa anafanya ulanguzi wa jezi zetu, Uwanja wa Taifa. "

Manara alisema wadau na mashabiki wa Simba, wanatakiwa kujipatia jezi za timu hiyo katika vituo vinavyotambulika.