Makwatta tegemeo la AFC Leopards ‘Ingwe’ kutupia mabao Ligi Kuu Kenya

Muktasari:

Mwaka uliofuatia 2017, Makwatta alisajiliwa na klabu ya Buildcon FC ya kule Zambia lakini alishindwa kutamba. Aliishia kujiunga na timu kadhaa za Uarabuni ikiwemo Al Nasr ya Dubai lakini bado soka la ugenini likamlemea.

Nairobi, Kenya. KABLA ya dirisha dogo la usajili la mwezi uliopita Januari kufungwa, aliyekuwa straika tegemeo wa AFC Leopards, John Mark Makwatta aliikacha klabu hiyo iliyosota kinoma na kwenda zake kujiunga na Zesco United ya Zambia.

Makwatta alikuwa na kila sababu ya kuondoka. Pale Ingwe maisha yalikuwa ni magumu sana kutokana na klabu kuwa inapitia hali ngumu ya kifedha kiasi kuwa kwa zaidi ya miezi minne sasa, imeshindwa kuwalipa wachezaji wake mishahara yao.

Wakati akiondoka licha ya hali hiyo ya msoto, Makwatta ndiye aliyekuwa akiongoza kwenye jedwali la vinara wa mabao msimu huu akiwa amecheka na nyavu mara 13.

Tangu alipoanza kucheza Ligi Kuu ya KPL 2015, hakuna msimu ambao Makwatta kaumaliza bila ya kuwa miongoni mwa wafungaji bora. Katika misimu yote hiyo kapachika mabao yasiyopungua 10.

ALITOKEA WAPI?

Kabla ya 2015, hakuna aliyekuwa akimfahamu hapa nchini katika ulimwengu wa soka hasa kwenye KPL. Kule angalau alikuwa ana kajina. Walikuwa tayari wameshaona uwezo wake.

Mwaka huo ambao ndio alijitangaza kwenye ligi ya KPL kuwa sio fowadi wa kimchezo mchezo na kumfanya kila shabiki wa soka la nyumbani kumtambua Makwatta alikuwa ana umri wa miaka 22 tu.

Soka lake alikuwa ameivisha akiwa shule ya upili na msingi kule Bungoma. Aliyechangia kumfua na kumgeuza kifaa  alicho sasa, ni kocha wake wa shule ya sekondari Luanda Okinyi aliyeanza kuwa nae tangu akiwa tineja.

Baada ya masomo yake, 2011  alijiunga na akademi ya JMJ Academy ambako alicheza kama kiungo mshambuliaji.

KIUNGO AGEUZWA STRAIKA

Klabu ya Nairobi City Stars kipindi hicho ikiwa inashiriki ligi ya KPL, ilimsajili na hapo ndipo kocha Mdachi Jan Koops aliamua kumbadilisha kutoka kiungo na kumgeuza kuwa straika.

Baada ya misimu mitatu, wanajeshi Ulinzi Stars walimsajili Oktoba 2013 kutoka City Stars. Msimu wake wa kwanza pale Ulinzi alitumika kama kiungo mshambuliaji.

Uliofuata wa 2015  Makwatta aligeuzwa  straika, alipoondoka fowadi tegemeo Stephen Waruru. Huo ukawa mwanzo wake wa kiu chake cha mabao.

DATA YA MAGOLI

Katika msimu huo wa 2015, Makwatta alimaliza akiwa mfungaji bora wa tatu. Makwatta alipachika mabao 14 kutokana na mechi 26, akimfuata Jesse Were aliyetia kimyani mabao 22 naye Michael Olunga akitwaa kiatu cha dhahabu kwa kufuma mabao 23.

Kwenye msimu wa 2016, Were na Olunga wakiwa wameondoka, ushindani wa kinara wa mabao katika ligi ukawa kati yake na Wycliffe Ochomo kipindi hicho akiichezea Muhoroni Youth. Kufikia mzunguko wa kwanza wa ligi, Ochomo alikuwa akiongoza kwenye ufungaji lakini kufikia mwisho wa msimu ni Makwatta aliyeibuka na kiatu cha dhahabu kwa kutinga mabao 15. Msimu huo alituzwa kuwa mchezaji bora vile vile

Mwaka uliofuatia 2017, Makwatta alisajiliwa na klabu ya Buildcon FC ya kule Zambia lakini alishindwa kutamba. Aliishia kujiunga na timu kadhaa za Uarabuni ikiwemo Al Nasr ya Dubai lakini bado soka la ugenini likamlemea.

Aliamua kurejea nyumbani na kujiunga na Ingwe Septemba 2019 na ameishia kuwa tegemeo kubwa kwao.

Kabla ya kutua Ingwe, mabingwa watetezi Gor Mahia walikuwa mbioni kumsajili ila mabosi wa Ingwe wakawachezea umafia chini ya maji na kupita naye kimya kimya.

Kilichotokea ni kwa mba baada ya Gor kumwasilisha ofa, Makwatta aliipigia simu menejimenti nya Ingwe na kuuliza ikiwa ingependa kumsajili.

Waliposema ndio, akawaelezea ofa aliyokuwa amepokea na hapo kwa kuwa walikuwa wakimhitaji kinoma, wakaamua kuipandisha dau lile.

“Huwa sipendi kuzungumziwa vitu ambavyo vimepita,” Makwatta alijibu alipoulizwa kuhusu ishu hiyo ya kuwatoka Gor.

Hadi anapondoka zake kwenda Zambia kwa mara nyingine tena wiki iliyopita, Makwatta alikuwa kinara wa magoli akiwa amepachika mabao 13. Kuondoka kwake kutampa unafuu Timothy Otieno na Enock Agwanda kufuzukia taji hilo.