Mabao ya Saliboko, Bocco anahusika buana!

Muktasari:

Katika hatua nyingine alimtaja nahodha wake Paul Nonga kuwa muunganiko wao katika nafasi ya ushjambuliaji pia imekuwa chachu ya mafanikio yao kufanya vizuri na kuamua matokeo ambayo yanaiweka timu yao kwenye nafasi nzuri.

MSHAMBULIAJI wa Lipuli FC, Daruweshi Saliboko amesema siri ya mafanikio na upambanaji katika nafasi anayocheza ni kufuata nyayo za nahodha wa Simba, John Bocco.

Saliboko ameingia kambani mara sita katika michezo tisa ya Ligi Kuu Bara ikiwamo hat trick aliyofunga majuzi dhidi ya Singida United na kumfanya awe mchezaji wa pili msimu huu kufunga mabao matatu katika mechi moja, mwingine akiwa ni Ditram Nchimbi wa Polisi Tanzania.

Amesema amekuwa akimfuatilia Bocco na kubaini mambo mengi yanayomuongezea morali ya upambanaji.

Alisema Bocco ni mmoja wa wachezaji wenye nidhamu mchezoni, mpambanaji na uwepo wake kwenye kikosi cha Simba kama nahodha unawapa matumaini ya ushindi kwa asilimia 40. “Majeraha kwenye mchezo ni sehemu ya changamoto, namuombea kwa Mwenyezi Mungu aweze kupona na kurudi kwenye majukumu yake ya kawaida, pia naamini kurudi kwake kutaongeza changamoto kwangu ya kupambana zaidi ili niweze kufikia mafanikio yake,” alisema.

“Unajua ukicheza na mtu unayemkubali hata kama ni timu mbili tofauti inakupa morali pale anapofanya vizuri na wewe unapambana ili ufanye vizuri zaidi yake, lakini kukaa kwake nje pia kunaniongeza nguvu za kupambana zaidi.”

Katika hatua nyingine alimtaja nahodha wake Paul Nonga kuwa muunganiko wao katika nafasi ya ushjambuliaji pia imekuwa chachu ya mafanikio yao kufanya vizuri na kuamua matokeo ambayo yanaiweka timu yao kwenye nafasi nzuri.

Alisema umoja na ushirikiano wao umekuwa sio wa kunyimana pasi pale mmoja wao anapokuwa kwenye nafasi nzuri ya kufunga na ndio siri ya mabao 12 waliyofunga.