Lampard njia nyeupe kutua Chelsea

Muktasari:

  •  Kiungo huyo wa zamani wa England, Lampard amecheza mechi 648 akiwa na Chelsea na kufanikiwa kunyakuwa mataji 11. 

London, England. Chelsea imepewa ruhusa ya kuzungumza na kocha wa Derby, Frank Lampard ili kuchukua nafasi ya kuifundisha klabu hiyo msimu ujao.

Lampard mwenye miaka 41, amecheza kwa miaka 13, Chelsea sasa anapewa nafasi kuchukua mikoba ya Maurizio Sarri, ambaye amejiunga na Juventus baada ya kukaa Stamford Bridge msimu mmoja.

Chelsea ‘The Blues’ imepanga kuwapa Derby kiasi cha pauni 4milioni kama wakimchukua Lampard.

"Wakati tunakaribia kuanza kwa msimu ni matumaini ta klabu zote mbili kuwa Chelsea itafikia mwisho wa suala hili," ilisomeka taarifa ya Derby.

"Klabu haitotoa maelezo mengine hadi suala hili litakapofikia mwisho."

Lampard alianza kibarua chake cha ukosa msimu uliopita akifanikiwa kuiongoza Derby kucheza mechi ya mtoano ya kupanda Ligi Kuu ambako walifungwa na Aston Villa.

Kiungo huyo wa zamani wa England amecheza mechi 648 akiwa na Chelsea na kufanikiwa kunyakuwa mataji 11.

Kama atafanikiwa kuchukua jukumu hilo ataanza kibarua chake wakati Chelsea ikiwa imefungiwa kusajili kwa misimu miwili na Fifa, lakini klabu hiyo imekata rufaa kwa mahakama ya usuluhishi wa michezo CAS.