Kaze: Nataka soka la kasi

Dar es Salaam. Kocha mpya wa Yanga, Cedric Kaze ameweka wazi kwamba katika maisha yake ya soka amekuwa muumini mkubwa wa soka la haraka na pasi za kwenda mbele ili kupata mabao.

Katika mazoezi yake ya juzi jioni (Jumapili), kocha huyo aliwataka wachezaji wake kuwa makini katika kufunga, zoezi ambalo alikuwa akilisimamia kwa umakini mkubwa.

Kocha huyo alitengeneza koni na kuweka wachezaji wawili eneo hilo, akionyesha ni jinsi gani anataka kufanya haraka kuirudisha Yanga katika ufungaji, huku akiimarisha makipa Metacha Mnata, Faruk Shikhalo na Ramadhan Kabwili.

Zoezi hilo hawakuwa wakihusika washambuliaji tu, bali wachezaji wote kwa pamoja walikuwa wakishiriki, huku kocha Kaze akiwasimamia na kuwabadilishia majukumu kila mara.

Kaze alisema ameanza kufurahishwa na namna ambavyo wachezaji wake wamekuwa wakiimarika na kumuelewa.

Ataanza kibarua chake cha kwanza Alhamis dhidi ya Polisi Tanzania, mchezo utakaofanyika Uwanja wa Uhuru, kisha KMC utakafanyika Uwanja wa CCM Kirumba.