KMC waanza vibaya Kanda ya Ziwa

Mchezaji wa Alliance FC David Richard akishangilia bao alilofunga leo dhidi ya KMC

IKIWA ni mchezo wa kwanza kwa KMC kucheza jijini hapa msimu huu wa Ligi Kuu Bara, safari yao ya kutafuta pointi sita imeanza vibaya kwani wamekubali kipigo cha bao 2-1 dhidi ya Alliance FC na kuacha alama zote tatu.
Katika mchezo huo uliopigwa Uwanja wa Nyamagana, Jahazi la KMC lilianza kuzamishwa  kipindi cha kwanza na beki wa Alliance, Geoffrey Luseke aliyefunga bao dakika ya 14 akimalizia mpira uliokuwa unazagaazagaa eneo la hatari.
Hata hivyo, Alliance waliendelea kufanya mashambulizi ya hapa na pale ambapo dakika ya 29, David Richard alifunga bao la pili akimalizia pasi ya Jerryson Tegete ndani ya 18.
KMC walipata bao la kufutia machozi dakika ya 75, Luseke alijifunga bao akijaribu kuokoa mpira wa hatari langoni kwao.
Licha ya kupata bao hilo ambalo ni kama zawadi waliyopata kutoka Alliance, KMC walishindwa kusawazisha bao la pili na kupelekea mechi kumalizika mabao 2-1.
KMC watacheza mechi nyingine ya ligi uwanja wa Nyamagana wiki ijayo ambapo watahitaji ushindi kutokana na timu hiyo kufanya vibaya.