KMC: Yanga tunajua pa kuwabana

JUZI Yanga ikiongozwa kwa mara ya kwanza na kocha wake mpya, Cedrick Kaze iliweza kuwatia adabu Polisi Tanzania kwa kuwalaza bao 1-0, lakini sasa hao KMC wamesema wamewaona wapinzani wao hao na kubaini wapi wawabane.

KMC ipo jijini Mwanza tangu juzi Jumatano ikiendelea kujifua kwa ajili ya mchezo wao wa kesho Jumapili dhidi ya Yanga, utakaopigwa CCM Kirumba.

Timu hizo zinakutana ikiwa Yanga inakumbuka ushindi dhidi ya Polisi Tanzania, huku KMC wakiambulia pointi moja mbele ya Ruvu Shooting, hivyo kufanya mechi hiyo kuwa ya upinzani mkali.

Hata hivyo, kazi kubwa itakuwa kwa makocha wa timu hizo, ambapo Kocha wa KMC, Habibu Kondo ndiye amemaliza kifungo chake cha mechi tatu na kufungua dhidi ya mabingwa hao wa kihistoria.

Kwa upande wa Yanga, Kaze atakuwa na kibarua kizito katika kudhihirisha uwezo wake kuendeleza ushindi ili kuwapa burudani mashabiki wake ambao kwa sasa wana matumaini ya kuona chama lao likitwaa ubingwa.

Akizungumza na Mwanaspoti, Kondo alisema vijana wake wanaendelea na matizi kwa ajili ya mchezo huo.