Hofu yatanda Genk, Samatta akisubiri majibu ya MRI

Muktasari:

Tangu kuanza kwa msimu huu wa 2019/20, Samatta ameifungia Genk mabao matano kwenye michezo  sita ya Ligi Kuu Ubelgi ambayo inafahamika zaidi kama Jupiler Pro.

Dar es Salaam. Nahodha wa timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’, Mbwana Samatta amefanyiwa uchunguzi wa kitabibu wa goti aligongwa wakati akiongoza Taifa Stars dhidi ya Burundi kwa mikwaju ya penalti 3-0.

Samatta aliyefunga bao la kuongoza kwa Stars kabla ya Burundi kusawazishwa, aliapa majeraha ya goti ambayo yalimlazimu kaimu kocha mkuu wa Taifa Stars ampumzishe na nafasi yake akaingia Himid Mao ‘Ninja’.

Akiwa na furaha ya ushindi baada ya kuwang’oa Burundi kwa mikwaju ya penalti, Samatta alirejea Ubelgiji kwenye klabu yake ya KRC Genk ambayo iliamua kumfanyia vipimo hivyo vya MRI jana.

Kwa kirefu ‘Magnetic resonance imaging’ MRI ni uchunguzi wa wa kisayansi unaotumia sumaku zenye nguvu, mawimbi ya redio, na kompyuta kutengeneza picha za kina ndani ya mwili.

Hivyo uchuguzi huo, uliofanyika kwa Samatta unatarajiwa kubainisha leo juu ya majeraha aliyoyapata nahodha huyo wa Taifa Stars kwenye mchezo dhidi ya Burundi ili waone ni kwa namna gani anaweza kupatiwa matibabu.

Kwa mujibu wa taarifa kutoka Ubelgiji ni kwamba joto la madaktari 10 ndio waliosimamia zoezi la Samatta kuchukuliwa vipimo hivyo licha ya yeye mwenyewe kujiona hana maumivu makubwa kwenye eneo hilo la goti.

Hofu imeanza kuzuka kwenye kikosi cha KRC Genk ambacho kinamtegemea mshambuliaji huyo kwenye Ligi ya Mabingwa Ulaya ambapo wataanza kutupa karata yao ya kwanza kwa kucheza na Salzburg, Septemba 17.

Novemba 2017, Samatta aliwahi kufanyiwa upasuaji wa goti kutokana na majeraha aliyoyapata pindi akiitumia klabu yake hiyo ambayo msimu uliopita aliisaidia kutwaa Ubingwa wa Ligi Kuu nchini humo huku akiifungia mabao 23.