Hans Poppe azua malumbano mahakamani

Muktasari:

Hans Poppe alikamatwa juzi Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere wakati akirejea nchini.

Dar es Salaam. Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili wa Klabu ya Simba, Zacharia Hanspope tayari yumo ndani ya Mahakama ya wazi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kwa ajili ya kusomewa mashtaka yanayomkabili,  lakini umeibuka  mvutano kati ya upande wa mashtaka na upande wa utetezi.

Upande wa Mashtaka kupitia kwa Wakili wa Serikali Mwandamizi, Shedrack Kimaro aliomba kuunganisha Hanspope katika kesi inayowakabili aliyekuwa rais wa Simba, Evans Aveva na Makamu wake, Godfrey Nyange maarufu Kaburu.

Hata hivyo, wakili wa Utetezi ukiongozwa Wandiba alipinga akidai kuwa mahakama ilishatoa uamuzi kuwa kesi iendelee kwa washtakiwa waliopo Mahakamani na kwamba kwa maombi hayo, mahakama inalengo la kirudisha nyuma kesi hiyo.

Hivyo, Wandiba ameomba Mahakama hiyo iendelee na kesi dhidi ya washtakiwa waliopo Mahakamani na Hanspoppe afunguliwe mashtaka yake.

Hakimu Mkazi Mkuu anayeshikiliza shauri hilo, Thomas Simba, baada ya kusikiliza hoja za pande zote, anandika uamuzi ama kukabiliana na upande wa mashtaka wa kumuunganisha Hanspoppe katika kesi ya akina Aveva au kutupilia mbali maombi hayo ya upande wa mashtaka.

Hanspope amefikishwa katika Mahakama hiyo, saa tatu na nusu na kupelekwa moja kwa moja katika chumba cha mahabusu wakisubiri kupandishwa kizimbani.

April 30, 2018, mahakama hiyo iliamuru washtakiwa Hanspoppe na Mfanyabiashara Frankly Lauwo wakamatwe popote walipo.

Mahakama hiyo ilitoa amri hiyo baada ya upande wa mashtaka kupitia kwa Wakili Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) Leonard Swai kuieleza kuwa wamewatafuta washtakiwa hao tangu Machi 16 mwaka huu bila mafanikio

Hata hivyo, Hanspope pekee ndio aliyekutwa Mahakamani na Takukuru.