Farid Mussa aziingiza vitani Yanga, Azam FC

Yanga na Azam zinawania saini ya winga aliyetemwa na CD Tenerife ya Hispania, Farid Mussa ambaye tayari yupo nchini.

Yanga wanaonekana kummezea mate winga huyo ambaye alifanya vizuri akiwa na timu ya Taifa Stars kwenye Fainali zilizopita za mataifa ya Afrika nchini Misri.

Farid alizaliwa Juni 21, 1996 mkoani Morogoro.

Alianza kucheza soka katika klabu ya Azam FC mwaka 2013. Aprili 2016, alikwenda nchini Hispania katika klabu ya CD Tenerife, na baada ya kuonyesha kiwango katika mechi za kirafiki, alisaini mkataba wa miaka miwili na kupelekwa katika timu ya wachezaji wa akiba inayoshiriki Ligi Daraja la Nne, Tercera Division.

Farid alicheza mechi yake ya kwanza Januari 14, 2017, akianza katika kikosi cha kwanza na kufunga bao la pili la timu yake katika sare ya 2–2 ugenini dhidi ya CF Union Viera.

Kisha Aprili 30, akafunga mabao mawili katika ushindi wa 5–1 ugenini dhidi ya UD Lanzarote.

Hata hivyo, maisha ya Farid Uhispania hayakumwendea kama alivyotaka na sasa amerejea nyumbani Tanzania

Farid pia ni mchezaji wa timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, ambayo aliitumikia kwa mara ya kwanza Novemba 9, 2013, akiingia kutokea benchini katika sare ya 0–0 ya mechi ya kirafiki dhidi ya Zimbabwe.