Dortmund yafuta mpango kumuuza Sancho Januari

Borussia Dortmund hawana mpango wa kumuuza Winga Jadon Sancho (20), katika dirisha dogo la usajili wa majira ya baridi kwenda klabu yoyote licha ya kuhusishwa na mpango wa kutua katika Klabu ya Manchester United.

Katika dirisha lililopita la usajili wa majira ya kiangazi, Sancho aliitesa Manchester United ambayo ilipeleka ofa mbili Dortmund ili kunasa huduma yake, lakini zilikataliwa na klabu hiyo kwa madai kwamba hazikufikia kiwango kilichohitajika.

Hata hivyo, wakati ddakika za lalasalama za dirisha hilo zikifika, mabingwa hao wa zamani wa Ligi Kuu England walituma ofa nyingine iliyokuwa mkwanja wa maana ambayo pia ilikataliwa.

Zipo tetesi kuwa vigogo barani Ulaya - Barcelona, Real Madrid na PSG zinajipanga kupigana vikumbo na Manchester United dirisha dogo litakapofunguliwa, ikielezwa pia Dortmund itakuwa tayari kumuachia kwa kuwa huenda ikamuuza kwa bei inayotaka kutokana na klabu hizo kuimarika kiuchumi.