Dele Alli ampasua kichwa Southgate

Muktasari:

Fowadi huyo Mwingereza ameonyesha kurejea kwenye kiwango bora cha soka lake akifunga mabao na kumfanya Southgate akubaliane na mtazamo wa Mourinho kwamba Alli hapaswi kuchezeshwa kwenye kiungo.

LONDON, ENGLAND . KOCHA mkuu wa England, Gareth Southgate amekiri kwamba kupanda kiwango cha Dele Alli tangu Jose Mourinho alipotua Tottenham Hotspur kunampasua sana kichwa kuhusu uteuzi wa kikosi katika kipindi hiki cha kueleeka michuano ya Euro 2020.

Alli alifunga mara mbili dhidi ya Bournemouth Jumamosi iliyopita, huku akiwa amefunga mabao matatu katika mechi mbili za mwisho akiwa chini ya Mourinho.

Fowadi huyo Mwingereza ameonyesha kurejea kwenye kiwango bora cha soka lake akifunga mabao na kumfanya Southgate akubaliane na mtazamo wa Mourinho kwamba Alli hapaswi kuchezeshwa kwenye kiungo.

“Jose anamchezesha kwenye namba 10 na imeonekana ni nafasi bora kwake, kwa sababu amekuwa na uhuru wa kukimbia ndani ya boksi,” alisema Southgate.

“Ni kitu kizuri amerudi kwenye ubora wake wa kufunga. Kwa sasa wachezaji wa Spurs wanapambana kujaribu kumshawishi kocha wao, lakini viwango vyao vikiwa vikubwa vinakuwa faida kubwa kwetu. Ukweli ni kwamba kumekuwa na ushindi mkubwa sana wa namba kwenye safu ya ushambuliaji. Hatukuwa na shida ya kufunga kwenye mechi za kufunga.”

England wanajipanga wakafanye kweli kwenye michuano hiyo ya Euro 2020 na kwenye kundi lao wamepangwa na Croatia, ambao ni mahasimu wao wa siku nyingi wakikutana mara kadhaa kwenye mechi kubwa huku vigogo wengine kwenye kundi lao ni Czech Republic.