Chelsea yamtega kimtindo Sarri

Muktasari:

Sarri alitua Chelsea kwa mkataba wa miaka mitatu kujaza nafasi ya Mtaliano mwenzake Antonio Conte aliyefukuzwa.

London, England. Chelsea imepania kufanya mapinduzi kwa kocha wake Maurizio Sarri anayehusishwa na mpango wa kutua Juventus.

Sarri anatarajiwa kuondoka Chelsea majira ya kiangazi baada ya kuinoa kwa msimu mmoja na kuipa tiketi ya kucheza Ligi ya Mabingwa Ulaya.

Lakini, Chelsea imekusudia kuanzisha mazungumzo na Mtalino huyo kuhakikisha anabaki Stamford Bridge msimu ujao.

Sarri ameweka bayana anataka kurejea katika Ligi Kuu Italia kujaza nafasi ya Maximilliano Alegri.

Juventus inataka kumtwaa kocha huyo wa zamani wa Napoli kutokana na ubora wake katika soka la Italia.

Hata hivyo, Chelsea ina amini itamshawishi Sarri kubaki Stamford Bridge msimu ujao, baada ya kufanya naye mazungumzo.

Sarri alitua Chelsea kwa mkataba wa miaka mitatu kujaza nafasi ya Mtaliano mwenzake Antonio Conte aliyefukuzwa.

Endapo mpango huo utagonga mwamba, Kocha wa Derby inayoshiriki Ligi Daraja la Kwanza Frank Lampard anaweza kujaza nafasi ya Sarri.

Lampard, (40), anapewa nafasi ya kureja Chelsea baada ya kufanya kazi nzuri Derby ambapo timu yake ilichapwa na Aston Villa katika mechi ya kupanda Ligi Kuu England.