Chanongo dili lake TP Mazembe lilikwama hapa

Muktasari:

Chanongo ni miongoni mwa wachezaji ambao wamepitia changamoto nyingi tangu yupo Simba ambako alijikuta akituhumiwa kila uchao kwamba yeye ni mnazi wa Yanga, jambo lililomfanya kuishi maisha magumu.

CHANGAMOTO ni sehemu ya maisha na wahenga wanasema huwezi kufikia mafanikio bila kupitia mitihani.

Walioyasema haya walikuwa na maana pana katika kuwatia moyo binadamu ambao tumeambiwa hatupaswi kukata tamaa kwa vile tu umegonga mwamba katika mipango yako.

Kikubwa unapokutana na changamoto ni kupambana na kutafuta jinsi ya kuzitatua na si kuzikimbia.

Kwa kweli hakuna mtu asiyepitia hizi changamoto lakini kikubwa kujizatiti kuzikabili kupambana nazo kadri walivyoweza na wengineo walifanikiwa kuzishinda.

Hii ni taswira tu ya jinsi vijana wa leo wanavyokutana na mitihani lakini wanapambana kuikabili kama ilivyokuwa kwa winga wa zamani wa Simba na Stand United, Haruna Chanongo, ambaye kwa sasa anakipiga Mtibwa Sugar.

Chanongo ni miongoni mwa wachezaji ambao wamepitia changamoto nyingi tangu yupo Simba ambako alijikuta akituhumiwa kila uchao kwamba yeye ni mnazi wa Yanga, jambo lililomfanya kuishi maisha magumu.

Hali hiyo ya kuonekana ni shabiki wa Yanga ilhali ni muajiriwa wa Simba ilisababisha kuona pa chungu ndani ya klabu hiyo na mwisho wake alitolewa kwa mkopo kwa Stand United msimu wa 2014/15.

Lakini, katika msimu wa kwanza alifanya vizuri hadi klabu kuvutiwa na kuamua kumsajili moja kwa moja baada ya Simba kufikia uamuzi wa kumuacha.

Licha ya kuaminika katika kikosi cha Stand United, lakini hakuwa chaguo la aliyekuwa kocha mkuu wa timu hiyo, Mfaransa Patrick Liewig.

Hiyo ilisababisha kijana huyo kuanza kusugua benchi pamoja na Elias Maguli aliyeamua kukimbilia nje ya nchi kwenda kujaribu kucheza soka la kulipwa katika timu ya Dhofar SC ya Oman na sasa anakipiga kwenye klabu ya Nakambala nchini Zambia.

Akizungumza na Mwanaspoti, Chanongo alifunguka kuwa kutokana na kuona hana maelewano na kocha aliamua kujiunga Mtibwa Sugar ambayo anaendelea kuitumikia hadi sasa.

ALICHEZA BURE UTD

Anasema makubaliano yake na Stand ilikuwa ni kupewa fedha ya usajili alipojiunga nayo, lakini ahadi hiyo haikutimizwa na ndio sababu iliyomtoa hapo na kujiunga na Mtibwa Sugar.

“Sikuchukua fedha yoyote kwao, nilisaini mkataba kwa kuwasikiliza tu maana nao ni binadamu na ni watu ninaowafahamu, waliniahidi wakiachiwa timu watanipa fedha yangu na mambo mengine kuendelea,” anasema.

TP MAZEMBE

Chanongo amefunguka kuwa majaribio ambayo alikuwa amefanya katikaKlabu ya TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) yalienda vizuri lakini uongozi wa timu yake ya zamani, Stand United ndio ulimbania.

Anasema katika majaribio hayoa mbayo alikuwa pamoja na beki wa kushoto wa Stand United, Abuu Ubwa, alifuzu lakini shida ilikuwa kwa uongozi wa Stand

United ambao haukuwa tayari kumua-chia.

“Nilifanya vizuri katika majaribio yale, tatizo lilikuwa kwa uongozi

wa timu yangu ambao haukutaka kuniachia na walihitaji fedha ambazo TP Mazembe haikuwa tayari kuzitoa. Wakala wangu aliona timu pale haina maslahi.

“Sasa najituma ili niweze kutoka zaidi ya hapa,” anasema.

ULAJI SIMBA

Chanongo anasema hakufikiria kurudi Simba licha ya klabu hiyo kuhitaji kumrudisha msimu huu.

Anasema kilichomharibia mchongo huo wa kurejea Msimbazi ni baadhi ya wanachama na mashabiki ambao hawana imani naye wakimtuhumu kuwa yeye ni shabiki wa mahasimu wao Yanga..

Anasema alikuwa katika wakati mgumu enzi yupo Simba kwa mitazamo ya kuwa yeye ana mapenzi na Yanga. Anasema hali hiyo ilisababisha kwenye mechi za Simba na Yanga hata acheze kwa kiwango gani ilikuwa kazi bure.

“Dah! Sina wazo la kurudi Simba, maana hata nikirudi Wanasimba hawana imani na mimi, sasa kwa hakika naweza kufanya vizuri kweli? Angalia nilikuwa naishi kwa hofu mno.

“Ukiangalia wengi waliniomba nirudi Simba hasa baadhi ya viongozi lakini nikifiria nilivyonyanyasika sikuwa na hamu ya kurudi tena,” alisema Chanongo ambaye anasema kwa sasa anafurahia maisha akiwa na Mtibwa Sugar.