Cabaye aanza mazoezi mdogomdogo

Muktasari:

Cabaye ni mmoja wa viungo wanaofanya vizuri katika kikosi cha Azam Fc.

KIUNGO wa Azam Fc, Masoud Abdallah 'Cabaye' amesema anaendelea vizuri na programu aliyoachiwa na daktari wake Mwanandi Mwankemwa ili kuwa fiti.
Cabaye alipata maumivu ya nyama za paja na kukaa nje ya uwanja, katika kipindi hiki cha Corona anatumia muda vizuri kujiweka fiti.
Kiungo huyo amesemahali yake imezidi kuimarika kadri siku zinavyokwenda jambo analomshukuru Mungu.
"Nashukuru kwamba hali iliyokuwa mwanzo ni tofauti na hivi sasa, naweza kufanya mazoezi vizuri ya viungo bila kupata maumivu yoyote kama mwanzo," alisema.
Aliongeza kwa kusema kipindi hiki cha Ligi kusimama pia kimekuwa na neema kwake kwani anatumia vizuri kuwa fiti kwa asilimia 100.
"Nitakuwa fiti tu na ndio maana naendelea kufata programu bila kusimama, ilikuwa programu ya wiki tano na mpaka hivi sasa nimefanya wiki tatu," alisema.