Bocco aanza mdogo mdogo
Muktasari:
Katika mazoezi ya leo asubuhi Bocco ambaye ni nahodha wa Simba, alikuwa karibu na kocha wa viungo Adel Zerane akimuelekeza baadhi ya mazoezi.
Mshambuliaji wa Simba, John Bocco amerejea katika kikosi cha timu hiyo, ambacho kinautumia Uwanja wa Gymkhana, Dar es Salaam kujiandaa na mchezo wa Ligi Kuu Bara dhidi ya Mtibwa Sugar, Septemba 13.
Bocco alipata majeraha ya goti katika mchezo wa Ligi ya Bingwa Afrika dhidi ya Ud Songo, Agosti 25 na alilazimika kukaa nje kwa takribani wiki tatu.
Katika mazoezi ya leo asubuhi Bocco alikuwa yupo karibu na kocha wa viungo Adel Zerane akimuelekeza baadhi ya mazoezi.
Mshambuliaji huyu hakujichanganya na mazoezi ya wechezaji wenzake bali alikuwa na programu za mazoezi ya viungo ambayo alikuwa akiyafanya kwa pembeni.
Urejeo wa Bocco katika kikosi hicho unatoa taswira nzuri katika benchi la ufundi baada ya mara kwa mara kocha mkuu, Patrick Aussems kusema kukosekana kwa mchezaji huyo kunaweka pengo katika kikosi chake.
Katika upande wa Ligi Kuu, Bocco aliukosa mchezo mmoja ambao ni dhidi ya JKT Tanzania ambao Simba waliibuka na ushindi wa mabao 3-1, uwanja wa uhuru.