Bao la Bocco lamfariji kocha Mayanja

Muktasari:

  • Bocco alifunga bao lake la kwanza msimu huu tangu ajiunge na Simba akitokea Azam katika mchezo dhidi ya Mwadui uliofanyika jana na Simba kushinda kwa mabao 3-0. Mabao mengine mawili ya wekundu wa Msimbazi yalifungwa na Emmanuel Okwi.

Kocha msaidizi wa Simba, Jackson Mayanja amefurahishwa na bao alilofunga mshambuliaji wake John Bocco'Adebayor' na kusema kuwa litampa kasi  mchezaji huyo ya kufunga zaidi.

Bocco alifunga bao lake la kwanza msimu huu tangu ajiunge na Simba akitokea Azam katika mchezo dhidi ya Mwadui uliofanyika jana na Simba kushinda kwa mabao 3-0. Mabao mengine mawili ya wekundu wa Msimbazi yalifungwa na Emmanuel Okwi.

Mayanja alisema tangu ajiunge na timu hiyo Bocco alikuwa hayuko vizuri kutokana na kusumbuliwa na majeruhi lakini kufunga bao hilo kutamrejesha mchezoni na anaamini atafanya vizuri zaidi katika michezo mingine ijayo.

 

"Amefunga bao zuri na naamini litampa morali ya kuzidi kufunga katika michezo ijayo. Amekuwa nje ya timu muda mrefu kutokana na majeruhi lakini amecheza mechi mbili na kufunga,ni jambo zuri"alisema Mayanja.

 

Simba iko nafasi ya pili kwenye msimamo wa Ligi Kuu ikiwa na pointi saba huku ikiwa timu inayoongoza kwa kufunga mabao mengi kwenye ligi hiyo baada ya kupachika nyavuni mabao 10.

 

Timu hiyo imeondoka leo alfajiri kwenda Mwanza kupambana na Mbao katika mchezo utakaofanyika Alhamis kwenye Uwanja wa CCM Kirumba.