Banda anyanyua makwapa Kusini

Muktasari:

  • Banda hakuwa sehemu ya kikosi hicho, kutokana na kutokuwa fiti sababu ya majeraha.

NDO hivyo tena. Licha ya kutokuwa sehemu ya kikosi cha Baroka FC kilichoitandika Orlando Pirates kwa mikwaju ya penalti, beki wa kimataifa wa Tanzania, Abdi Banda ametwaa ubingwa wake wa kwanza Afrika Kusini.

Baroka imetawazwa kuwa mabingwa wa Telkom baada ya kuifunga Orlando Pirates ya Milutin Sredojevic ‘Micho’ kwa penalti 3-2, baada ya sare ya mabao 2-2.

Banda hakuwa sehemu ya kikosi hicho, kutokana na kutokuwa fiti sababu ya majeraha.

Beki huyo, aliishuhudia akiwa jukwani Baroka ikiweka rekodi ya kuwa timu ya kwanza kutoka Limpopo kushinda taji hilo.

Baada ya kutwaa ubingwa huo wa Telkom, kesho Jumanne Baroka itakuwa ugenini kucheza mchezo wa Ligi Kuu Afrika Kusini ‘PSL’ dhidi ya Mamelodi Sundowns.

Baroka itaingia kwenye mchezo huo ikiwa na urejeo wa Banda kwenye kikosi chake lakini pia na kumbukumbu ya kuitandika Mamelodi kwenye robo fainali ya Telkom kwa mabao 2-0.