Azam yaishusha Yanga, yaandika historia mpya

Muktasari:

Kabla ya mechi na Singida United, Azam ilikuwa na rekodi ya kushinda mabao 6-1 dhidi ya JKT Tanzania na Villa Squad 6-2

Azam FC imepanda nafasi ya pili baada ya kushusha kipigo cha mabao 7-0 dhidi ya Sinida United na kuwashusha Yanga ambao walitoka suluhu katika mechi yao leo jioni dhidi ya Biashara.

Ushindi huo unawafanya kuandika historia mpya ya kushinda mabao mengi katika mechi moja tangu walivyofanya hivyo kwa JKT Tanzania kwa kuifunga mabao 6-1 msimu wa 2018/2019.

Mabao manne ya Obrey Chirwa, mawili ya Idd Nado na moja la kujifunga na David Natley yametosha kuipa alama tatu wana lamba lamba kwenye mechi iliyopigwa Uwanja wa Azam Complex na kufikisha pointi 62.

Azam walitawala mpira muda mwingi na kulisakama lango la wapinzani wao kiasi cha kupata nafasi nyingi za kufunga mabao mengi ila hawakuzitumia vizuri.

Baada mabao kuzidi kocha wa Singida, Ramadhan Nswanzurwimo aliamua kumtoa kipa aliyeanza, Owen Chaima na kumuingiza mwingine ambaye hakuruhusu bao hadi mpira unaisha.

Yanga na Azam wamebakiwa na mechi tano kumaliza msimu huu ambazo wote wanazitolea macho kuhakikisha wanasalia nafasi ya pili.