Arteta aokoa hela za Arsenal kwa Ozil

LONDON, ENGLAND. KOCHA, Mikel Arteta ameripotiwa kuokoa pesa kibao za Arsenal kutokana na uamuzi wake wa kumpiga benchi Mesut Ozil.

Kocha huyo Mhispaniola hajampanga kiungo huyo wa Kijerumani katika mechi yoyote ya msimu huu na mechi yake ya mwisho ya ushindani kucheza ilikuwa Machi.

Ozil ameondoshwa pia kwenye orodha ya wachezaji 25 wa Arsenal watakaocheza Europa League na kuna uwezekano akawekwa kando katika kikosi cha Ligi Kuu England.

Tatizo la kiuchumi liliwafanya Arsenal kupunguza wafanyakazi 55 wasiokuwa wachezaji kwenye dirisha lililopita la uhamisho wa majira ya kiangazi, licha ya kwamba Ozil alipingana na jambo hilo. Mshindi huo wa Kombe la Dunia, analipwa Pauni 350,000 kwa wiki na hivi karibuni alitoa ofa ya kumlipa mshahara maskoti wa Arsenal, Gunnersaurus baada ya klabu kudai haina pesa na inamwondoa kazini.

Kwa mujibu wa The Athletic, Arsenal imemlipa staa huyo wa zamani wa Real Madrid bonasi ya Pauni 8 milioni mwezi uliopita kutokana na kuendelea kubaki Emirates. Lakini, inadaiwa Arsenal imeokoa pesa nyingi kwa Ozil kutocheza.

Imeelezwa kwamba kiungo huyo wa zamani wa Schalke anapaswa kulipwa bonasi kila mechi atakayocheza kutokana na kipengele kwenye mkataba wake.