Ame arejea kikosini Simba

BEKI wa kati wa Simba, Ibrahim Ame amepona majeraha yake ya goti na mkono wa kulia ambavyo aliumia katika mechi ya kirafiki na Mlandege ambayo iliyochezwa Oktoba 17, 2020 Uwanja wa Azam Complex.

Ame baada ya kupona ameanza mazoezi na wachezaji wenzake tofauti na ilivyokuwa wakati anaumwa alikuwa akifanya mazoezi mwenyewe pembeni ya uwanja huku akiwa anasimamiwa na kocha wa viungo, Adel Zrane.

Baada ya kurejea katika kikosi hiko chenye mabeki wanne wa kati, Erasto Nyoni, Pascal Wawa na Joash Onyango, Ame ataendelea kukutana na ushindani wa kuwania nafasi ya kucheza huku mwenyewe akieleza hakuna timu ambayo inakosa ushindani hata nyuma alipoanza maisha ya soka ilikutana nalo hilo.

Ame anasema hata wakati anajiunga na Coastal Union, alikuwa anakutana na hilo kwahiyo hata hapo Simba itatokea siku anaweza kupata nafasi mbele ya wazoefu hao watatu.

"Kiukweli kabisa najifunza mambo mengi kutoka kwa Nyoni, Onyango na Wawa ambao kwangu natamani kufanya kwanza kama wao ili niongeze na vyangu ili kuwa zaidi na hapo ndio naimani nitapata nafasi ya kucheza," anasema Ame na kukubali ushindani upo tena wa kutosha.

"Ukiangalia katika kikosi chetu ushindani haupo katika nafasi ambayo nacheza mimi bali katika kila nafasi moja kuna wachezaji si chini ya wawili wenye viwango bora na kuna wakati tunacheza kwa kupishana," anasema Ame.