Aguero kumpisha Messi Man City

MANCHESTER, ENGLAND. STRAIKA, Sergio Aguero huenda akaamua kuachana na Manchester City ili kufungua milango ya Lionel Messi kutua Etihad. Muargentina huyo amekosekana uwanjani kutokana na majeruhi na hakuna ubishi chama hilo la Pep Guardiola linamisi huduma yake. Kwa sasa yupo kwenye mwaka wa mwisho wa mkataba wake huku Inter Milan wakitazama namna ya kumnasa.

Inter wapo tayari kumpa ofa ya mkataba wa miaka miwili staa huyo wa zamani wa Atletico Madrid, wakipoambana kujaribu kumaliza utawala wa Juventus kwenye soka la Italia.

Na Man City wapo tayari kumwaacha Aguero aondoke bila ya kuweka ugumu wowote ili kufungua milango ya Messi kutua kwenye kikosi hicho cha Etihad. Messi mkataba wake utafika tamati mwishoni mwa msimu huu na kuna dalili zote akaondoka Barcelona ambako hana furaha.