Yanga kuivutia pumzi Coastal kwa KMKM

Muktasari:

Kikosi cha KMKM kinatarajia kushuka dimbani kesho kumenyana na Yanga kwenye mchezo wa kirafiki unaotarajia kuchezwa kwenye uwanja wa Azam Complex Chamazi saa moja usiku.

 

 

YANGA kesho Jumatano watacheza mechi ya kirafiki dhidi ya KMKM  ya kisiwani Unguja, Zanzibar, mechi hiyo itachezwa Uwanja wa Azam Complex, Chamazi jiji Dar es Salaam.

Yanga watatumia mechi hiyo kujiandaa na mchezo wa raundi ya tano ya mzunguko wa Ligi Kuu Bara itakayochezwa Oktoba 3, 2020, Jumamosi kwenye Uwanja wa Mkapa.

Beki wa zamani wa Yanga, Haji Mwinyi ameiambia Mwanaspoti Online wamejiandaa vizuri kucheza na Yanga ikiwa ni maandalizi ya Ligi ya Kuu Zanzibar inayotarajia kuanza hivi karibuni.

 "Ni miongoni mwa wachezaji ambao tunakuja Dar es Salaam leo Jumanne, tunatarajia mchezo mzuri kutoka Yanga na naamini ni mchezo ambao utatupa matokeo ya kikosi chetu kina mapungufu sehemu gani,"

 "Nimecheza Yanga lakini kwa asilimia kubwa natarajia kukutana na nyota wengi wapya kwani niliocheza nao wengi wameondoka kikosini ni wachache sana waliobaki hivyo kwasasa mimi pia ni mgeni kwa timu hiyo," amesema Haji.

 Haji ameongeza kuwa anajua ubora wa nyota waliobaki kama Haruna Niyonzima, Deus Kaseke na wengine aliocheza nao hivyo amewapa mbinu wenzake kama watacheza na nyota hao wajue namna ya kuwazuia.