Biashara Utd wawafokea Simba!

Muktasari:

MASTAA wa Biashara United wametamka wazi kwamba hawana mchecheto wowote dhidi ya Simba, kesho Jumapili kwenye Uwanja wa Mkapa.

MASTAA wa Biashara United wametamka wazi kwamba hawana mchecheto wowote dhidi ya Simba, kesho Jumapili kwenye Uwanja wa Mkapa.

Biashara wana pointi sita huku mabingwa hao watetezi wakiwa na alama nne, jambo ambalo litafanya mchezo huo uwe mgumu kwa timu hizo mbili.

Nahodha wa kikosi hicho, Abdulmajid Mangalo alisema wanajua ugumu wa mchezo huo lakini wanachotaka ni kuendeleza wimbi la ushindi hivyo wamejipanga kuwakabili Simba.

“Tunahitaji ushindi katika huu mchezo, tuko fiti kuwakabili Simba, tunajua ugumu wa pambano hili lakini tumejipanga sisi kama wachezaji kuweza kupata pointi tatu,

“Hatujawahi kupata ushindi kwenye Uwanja wa Taifa hivyo tumejipanga kuhakikisha kwa mara ya kwanza tunawafunga Simba katika huu mchezo maana hatujawahi kuwafunga tangu tumepanda Ligi Kuu,” alisema Mangalo.

Kiungo Ramadhani Chombo ‘Redondo’ alisema watawaheshimu Simba katika pambano hilo hivyo wataingia kwa umakini mkubwa ili kuweza kuondoka na pointi tatu kwenye mchezo huo mgumu.

“Tutakutana na timu kubwa hivyo ni muhimu kucheza kwa nidhamu kubwa,” alisema Redondo.