Ben Pol: 2020 ni wa kufanya maajabu

Muktasari:

Mashabiki waliokuwa wanaelekeza mashambulizi kwa Ben Pol kama amezama kwenye mapenzi kuliko kazi, basi watarajie kuona makubwa kutoka kwa msani huyo ndani ya mwaka huu

MSANII wa Bongo fleva, Ben Pol amesema mwaka huu 2020 ni wa kuangalia wale ambao wanafanya maajabu kwenye sekta zao na sio kuruhusu kejeli zinazoelekezwa kwake.

 

Tangu aingie kwenye mahusiano na Mkenya Anerlisa, mashabiki wamekuwa wanamuona amezama zaidi mapenzini kuliko muziki jambo ambalo amelikana.

 

Amesema kwa sasa hataruhusu kukaribisha maneno ya kumvunja moyo, bali ataelekeza nguvu zake kufanya vitu vikubwa anavyoamini vitabadili upepo wao.

 

"Mfano Mbwana Samatta angeamua kusikiliza kila neno la mtu anayemtazama kama kioo sidhani kama angefikia hatua aliopo, alikuwa anaangalia melengo yake ndio maana kila mtu anamuona anapeperusha bendera ya taifa,"

 

"Nimegundua ukiona shambulizi linaelekezwa kwako basi ujue una kitu kikubwa ambacho unatakiwa kuongeza juhudi ili kazi zako ziwe bora zaidi, nimetolea mfano Samatta asingejituma asingekuwa anapata sifa kama anazopata kwa sasa,"amesema.

 

Amesema anaamini mwaka huu utakuwa wa mafanikio ya kimuziki kwake ambapo anapanga kutembea mikoa yote ya Tanzania kukutana na wadau wake.

 

"Mwaka huu utakuwa wa tofauti kwangu, nitatembea Tanzania nzima, nitakutana na watoto yatima, wazee na makundi mbalimbali yenye uhitaji, naamini nitakuja na kitu tofauti,"amesema.