Refa aimaliza Yanga Cairo

MABINGWA wa Kihistoria wa Tanzania, Yanga usiku huu imekamilisha safari ya siku 86 kwenye michuano ya kimataifa baada ya kubabuliwa mabao 3-0, huku wachezaji na hata benchi la ufundi likimlalamikia mwamuzi aliyelichezea pambano lao na Pyramids ya Misri.
Yanga iliyokuwa ikisaka ushindi usiopungua mabao 2-0, ilijikuta ikiaga michuano hiyo kwenye Uwanja wa Juni 30 kwa kufungwa mabao 3-0 katika mchezo ambao ilishuhudiwa Kocha Mwinyi Zahera akiwaanzisha kikosi cha kwanza kwa Deus Kaseke na Juma Balinya, huku beki Lamine Moro akirejea kikosini kutoka kutumika adhabu ya kadi nyekundu aliyopewa kwenye mchezo dhidi ya Zesco United ya Zambia katika mechi ya awali wa raundi ya kwanza ya Ligi ya Mabingwa Afrika.
Katika mchezo hio kipa Farouk Shikhalo alifanya kazi ya ziada kuokoa michomo hatari ya nyota wa Pyramids walioongozwa na nahodha wao, Abdalla El Said na Eric Traore aliyeifungia wenyeji bao dakika ya 28 akimalizia mpira wa faulo wa El Said kuokolewa na Farouk naye kuukwamisha wavuni.
Bao hilo lililalamikiwa na wachezaji wa Yanga wakidai ilionekana kama mfungaji alikuwa ameotea, lakini mwamuzi wa mchezo huo aliyeonekana kama akiiuma Yanga kwa muda mrefu alikomalia msimamo wao na mchezo kuendelea na Vijana wa Jangwani kwenda mapumziko wakiwa nyuma.
Kipindi cha pili Zahera alimtoa Abdulaziz Makame na kumuingiza Feisal Salum kabla ya kumtoa Balinya na kumuingiza Patrick Sibomana na baadaye Jaffar Mohammed aliingia kziba nafasi ya Ali Ali aliyeumia dakika ya 70 baada ya kuruka juu ya kutegewa mgongo na mchezaji wa Pyramids na kujikuta akianguka vibaya na kutolewa uwanjani na kigari cha watu wa huduma ya kwanza.
Dakika ya 80 kocha ya El Said iliunganishwa wavuni na Mohammed Farouk na kuikatisha tamaa Yanga kabla ya Yanga kupata pigo tena baadfa ya Lamine Moro kuumia na kutolewa uwanjani dakika ya 85, huku ikiwa imeshamaliza idadi ya wachezaji wa kuwabadilisha.
Dakika za nyongeza, Yanga ilishukizwa ikifungwa bao la tatu kupitia kwa El Said tena baada ya mabkei wake kuzembea kumkaba John Antwi aliyeingia kipindi cha pili aliyekimbia na mpira kabla ya kutoa pasi kwa mfungaji aliyemtungua kirahisi Shikhalo.
Katika mchezo huo Yanga ilishuhudia nyota wake wakionyeshwa kadi za njano akiwamo Lamine dkika ya 26, Ally Mtoni 'Sonso'(dk55), Feisal Salum (dk 71').
Kwa kipigo hicho, Yanga imejikuta ikitolewa kwa jumla la mabao 5-1 na kuungana na Simba, KMC na Azam Fc zilizotolewa mapema kwenye michuano ya Ligi ya Mabingwa na Kombe la Shirikisho.
Kikosi Yanga:
Shikhalo, Abdul, Sonso, Ali, Lamine, Makame, Kaseke, Tshishimbi,  Urikhob, Balinya na Balama.