Babu Seya awataka Nyoshi, Patcho Mwamba kuifufua FM Academia

Muktasari:

Anawaomba Nyoshi na Patcho warudi katika bendi moja ili waweze kufanya kazi kwa pamoja, kwani kulikuwa na ushawishi wa wao katika muziki wa dansi.

Dar es Salaam. Mwanamuziki Nguza Viking ‘Babu Seya’ amesema wanamuziki wa dansi Nyoshi El Saadat na Patcho Mwamba hawakutakiwa kutengana amewataka warudi kufanya kazi kwa pamoja kama zamani.

Nguza Viking amesema hayo kuwa Septemba 10, 2019 Bahari Beach jijini Dar es Salaam kutengana kwao hakujaleta kuinua muziki wa dansi bali wameushusha kwani hakuna hata mmoja anayefanya vizuri katika muziki kwa sasa.

“Mfano tukiwazungumzia Nyoshi na Patcho, kwanza mimi binafsi nisingependa hawa watu watengane katika bendi ya Fm Academia, sababu nimeona kabisa utengano wao umewapoteza kwani hakuna wanachokifanya katika bendi zao na hata kuunyanyua muziki wa dansi bali wameushusha tu,” alisema Nguza Viking.

Aidha Nguza Viking alisema anawaomba Nyoshi na Patcho warudi katika bendi moja ili waweze kufanya kazi kwa pamoja, kwani kulikuwa na ushawishi wa wao katika muziki wa dansi.

Nyoshi na Patcho walikuwa katika bendi moja ya Fm Academia iliyokuwa inaogozwa na Nyoshi akiwa kama Rais wa bendi hiyo na baadae alikuja kuvuliwa urais na kupewa Patcho Mwamba ambaye hadi sasa ni Rais wa bendi hiyo.

Baada ya kitendo hicho Nyoshi alijiengua Fm Academia na kuunda bendi yake ya Bogoss Musica.